MAELFU ya wakazi wa mji wa Songea mkoani
Ruvuma, jana walifurika katika uwanja wa Matalawe kuhudhuria mkutano wa
kampeni wa mgombea urais wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema)
chini ya mwamvuli wa Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa), Edward
Lowassa.
Hali hiyo ilitokea mjini Songea jana
jioni wakati Lowassa alipowasili akitokea Mkoa wa Njombe alikohutubia
mikutano miwili ya hadhara juzi katika miji ya Makambako na Njombe.
Wakati wa mapokezi ya mgombea huyo mjini
hapa, walikuwapo mamia ya vijana, akina mama, wazee na watoto ambapo
walijipanga barabarani wakimsubiri awasili uwanjani hapo.
Mbali na maelfu ya wananchi waliokuwa
barabarani, idadi kubwa ilikuwa uwanjani hapo huku kila mmoja akiwa na
hamu ya kumwona mgombea huyo. Kutokana na hali hiyo, shughuli za kijamii
kama maduka, baa na masoko, zilisimama kwa muda kwa kuwa wananchi wengi
walikuwa wakimpokea Lowassa.
Wakati hayo yakiendelea, makundi ya
vijana walikuwa wamepanda katika miti inayozunguka uwanja huo ulio
jirani na shule za msingi za Matalawe na Mnazi Mmoja. Kutokana na wingi
wa watu, baadhi ya vijana walilazimika kupanda katika moja ya madarasa
ya jengo la Shule ya Msingi Mwembechai ambapo paa la jengo hilo
lilinusurika kuporomoka baada ya kuzidiwa na uzito.
Akihutubia mkutano huo, Lowassa aliahidi
kulijenga paa hilo baada ya kugundua uwepo wa tatizo hilo. Pamoja na
hayo, alisema atakapoingia madarakani, ataiangalia mikataba yote ya
madini ili kuona inavyowanufaisha Watanzania.
“Hata wakubwa huko walielewe hili,
simaanishi kwamba nawatisha wawekezaji, bali nayasema haya kwa sababu
hatuwezi kuwa na madini na gesi ya kuinufaisha dunia wakati Watanzania
hawana ajira. “Hata deni la Taifa nitaliangalia ili tuone
lilivyopatikana na jinsi lilivyotumika.
Hata kile kiwanda chenu cha tumbaku,
nitakifufua ikiwa ni pamoja na kuwaletea umeme wa uhakika hapa Songea,”
alisema. Awali akihutubia wananchi wa Jimbo la Madaba mkoani hapa,
Lowassa aliwataka wanaomkosoa kuhusu utendaji wake, wajibu hoja badala
ya kuongea maneno yasiyokuwa na msingi.
“Hao wenzetu wasipige kelele, wajibu
hoja kwa sababu mimi tatizo langu ni umasikini wa Watanzania. Kama wana
njia mbadala ya kuondoa umasikini waseme, wasipige kelele tu,” alisema
Lowassa.
Akizungumzia kilimo, alisema
atakapofanikiwa kuingia madarakani, pamoja na kuahidi kufuta kodi zote
katika sekta hiyo, Serikali yake haitawakopa wakulima na kwamba ikitokea
wakiwakopa, watakapolipwa watalipwa na fidia kama sehemu ya kuwainua.
Kuhusu kero ya umeme ambayo imekuwa
ikiwasumbua wananchi wa Ruvuma kwa muda mrefu, alisema atakapoingia
madarakani atapeleka umeme katika Jimbo la Madimba.
SUMAYE Naye Waziri Mkuu mstaafu,
Frederick Sumaye, alisema mwaka huu ndiyo mwaka wa kuiondoa CCM
madarakani kwa kuwa matatizo waliyonayo Watanzania hayawezi kuondoka
kama chama hicho kitaendelea kutawala. “Huu ndiyo mwaka wetu wa kufanya
mabadiliko, na nawaambia kama msipokubali kuiondoa CCM madarakani kwa
kuipigia kura Chadema na wagombea wa Ukawa, maisha yenu yataendelea kuwa
mabaya.
“Haiwezekani nchi hii ikaendelea kuwa
masikini, nawaambia umasikini tulionao ni wa kujitakia. “Msimchague
Magufuli kwa sababu hana nia njema na Watanzania, na ndiyo maana hata
alipokuja hapa juzi akielekea Ludewa, barabara hii ilimwagiwa maji ili
asipate vumbi,” alisema Sumaye.
Pia, alisema viongozi wa CCM
wanaomchafua Lowassa hawana hoja za msingi bali wanafanya hivyo kwa kuwa
wanamwogopa. Sumaye aliwataka Watanzania wasiogope kufanya mabadiliko
ya uongozi kwani kitendo chake na Lowassa kuhamia Ukawa ni kielelezo cha
kutaka kuimarisha demokrasia wakiwa nje ya CCM
Post a Comment