Featured
    KWA HABARI NA MATANGAZO EMAIL : pbuyegu2@gmail.com ... Get a superior results by advertising with us by E- Mail us pbuyegu2@gmail.com We will bring Your Business to Light

    Featured Posts

Loading...

Zitto Kabwe akanusha tuhuma dhidi ya Dk. Mengi...Asema wanaomhusisha ni walioumbuliwa na PAC

 

Siku moja tu baada ya Mwenyekiti Mtendaji wa IPP, Dk. Reginald Mengi, kutangaza usalama wa maisha yake kuwa hatarini, kiongozi wa Chama cha ACT-Wazalendo, Zitto Kabwe, ameibuka na kudai tuhuma alizohusishwa dhidi ya Mengi si za kweli.

Dk. Mengi, alitangaza hofu yake juzi, wakati alipokutana na vyombo mbalimbali vya habari, kufuatia gazeti moja linalochapishwa kila wiki kuandika kuwa Rais Jakaya Kikwete, ameahidi kupambana na Mengi baada ya kuelezwa kuwa anaihujumu serikali yake.

Zitto alihusishwa katika habari hiyo kuwa ndiye anayedaiwa kwenda kwa Rais Kikwete kumweleza kuwa  Mengi anaihujumu serikali yake baada ya kutolewa kwa ripoti ya PAC.

Alisema taarifa maalum ya Kamati ya Bunge Hesabu za Serikali (PAC), kuhusu ufisadi wa Sh. Bilioni 306 za Escrow, haihusiani kwa namna yoyote na Dk. Mengi.

Zitto alisema kuwa watu wanaomhusisha mfanyabiashara huyo na mkakati wa kuihujumu serikali ya Rais Kikwete ni wale waliokosa hoja baada ya masuala yao ya kuwahujumu Watanzania kukwama kufuatia ripoti ya PAC kuwaumbua.
 
Zitto alitoa kauli hiyo jana katika uwanja wa mahakama ya Mwanzo mjini Shinyanga.

Katika hofu yake, Dk. Mengi alisema ameshangazwa na ukimya wa Ikulu na Idara ya Habari Maelezo, pamoja na habari hiyo kuchapishwa kwenye gazeti ikimhusisha Rais.

 "Mengi sio mbunge, sio mjumbe wa PAC na hakushawishi PAC kwa namna yeyote ile. Wezi wa Escrow wasitapetape kutafuta mchawi wakati mchawi ni wizi wao wenyewe," alisema Zitto.

"Habari zilizoandikwa kwenye gazeti la Taifa Imara zinazomhusu  Regnald Mengi na Rais Jakaya Kikwete si za kweli, ni fitina zimetengenezwa," alisema.

Zitto, aliyekuwa Mwenyekiti wa PAC, alisema habari iliyoandikwa na gazeti la Taifa Imara la Machi 23, mwaka huu, zinazoonyesha kuwa alikutana na Rais kwa msaada wa watu mbalimbali, ni mwendelezo mwingine wa porojo za watu walioathiriwa na uamuzi wa PAC katika sakata la Escrow.

"Habari hiyo ilibeba maudhui ya 'post' iliyoandikwa katika mtandao wa Mwanahalisi online, inaonyesha kuwa mimi nilikutana na Rais kwa msaada wa watu mbalimbali na katika kikao hicho inadaiwa nilisema kuwa Mengi ndiye aliyechochea wabunge kuishughulikia serikali ya Rais Kikwete ili ianguke,” alisema.

Zitto alisema hahitaji  kutumia watu kwa ajili ya kukutana na Rais Kikwete, kwa kuwa suala hilo linawezekana kufanyika katika taratibu za kawaida za kiserikali.

Alisema kitendo cha gazeti hilo kudai kuwa aliomba watu wamkutanishe na Rais, inaonyesha namna mwandishi alivyoshindwa kutunga uongo wake.
 
“Hadithi ya kwamba nimeomba watu wanikutanishe na Rais inaonyesha namna mwandishi alivyoshindwa kutunga uongo wake.

Katika kukutana kwangu na Rais kikazi sijawahi hata mara moja kuzungumzia watu. Hivyo kusema nilikwenda Ikulu kumzungumzia  Mengi ni kunidharau na kuidhalilisha Taarifa ya Urais,” alisema.

Alisema ifahamike kuwa gazeti la Taifa Imara linamilikiwa na James Rugemalira wa kashfa ya Escrow na kuendeshwa na Prince Bagenda, aliyeandaa mkutano wa mmoja wa mawaziri waliofukuzwa kazi kwa kashfa hiyo.

Aliongeza kuwa hata chanzo cha habari hiyo ni mtandao wa Mwanahalisi online ambao unaoendeshwa na mmiliki wa Mawio, gazeti ambalo kila wiki lina habari za kutunga dhidi yake na chama chake.

Aidha, alisema kama kuna mtu ana chembe ya ushahidi wa jambo hilo apeleke kwenye vyombo vya dola kwa hatua kuliko kurudia rudia porojo hizo kwenye vyombo vya habari.

Alisema kwa sababu hiyo amemwelekeza mwanasheria wake achukue hatua za kisheria dhidi ya gazeti la Taifa Imara na gazeti la Mawio, kwa mfululizo wa habari za kutunga uongo dhidi yake kila kukicha.

Juzi  Mengi alitoa taarifa katika vyombo vya habari akielezea hofu yake juu ya ukimya wa Kurugenzi ya Mawasiliano Ikulu, pamoja na Idara ya habari maelezo kufuatia taarifa iliyoandikwa na gazeti la Taifa Imara la Machi 23 mwaka huu.

Mwandishi alizungumza  kwa njia ya simu na Mkurugenzi wa Habari Maelezo, Assah Mwambene, na kujibu kwa mkato "no comment my dear" (sina cha kuzungumza).
Download Our App

Post a Comment

CodeNirvana

BLOG RAFIKI

© Copyright EMMANUEL SHILATU - BREAKING NEWS BLOG
Back To Top