KITENDO cha
aliyekuwa Mbunge wa Kigoma Kaskazini, Kabwe Zitto, kutangaza bungeni kuwa
anang’atuka ubunge, kilisababisha Bunge kuzizima huku akipewa pole na wabunge
wengi.
Hata hivyo
mwanasheria wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Tundu Lissu na
alikacha kumpa mkono.
Zitto ambaye
alisoma barua aliyomwandikia Spika Anne Makinda, kuwa analazimika kuachia
wadhifa wa ubunge baada ya chama chake kutangazia umma kuwa sio mwanachama wao,
kulisababisha simanzi kwa wabunge wengi ambao baada ya kikao cha Bunge
kusitishwa wengi walienda kumpa pole.
Hata hivyo,
Zitto ambaye alikuwa amekaa pamoja na wabunge wengine wa Chadema ambao wengi wao
walimkumbatia kama ishara ya kumpa pole na kumtakia kila la heri aendako, Lissu
na Msigwa waligoma kumpa mkono mbunge huyo.
Kitendo cha
Lissu na Msigwa kukacha kumpa mkono Zitto, kiliwafanya baadhi ya wabunge kupigwa
na butwaa, lakini hata hivyo Lissu alipoulizwa kwa nini hakumpa mkono mbunge
mwenzake huyo, ambaye wametumika pamoja kwenye chama cha Chadema kama viongozi,
alisema yeye sio mnafiki.
Msimamo wa Zitto
Zitto aliliambia Bunge kuwa licha ya kutopokea barua rasmi ya kumjulisha juu ya
uamuzi wa kumtimua uanachama, ameona ni vyema akachukua uamuzi huo mapema kwa
sababu jamii inaamini kwamba yeye sio mwanachama wa Chadema.
“Nashukuru,
ushirikiano nilioupata kwa Bunge la Tisa na la 10, limenijenga na kunifanya
niwatumikie Watanzania kwa kiwango nilichostahili. “Naondoka katika Bunge hili
lakini naamini nitarudi tena kwa mapenzi ya Mungu na tunaweza kuonana mwezi
Novemba,” alisema.
Kuhusu mafao
mbalimbali anayostahili kupata kutokana na utumishi wake kwa Bunge, alisema hilo
kwake si muhimu na akaendelea kukumbusha kuwa kama Watanzania wanakumbuka ni
siku nyingi yeye aliomba kuondolewa posho mbalimbali, ili ziende kusaidia
Watanzania wenye shida.
“Suala la mafao
kwa sasa kwangu si kipaumbele, cha msingi niende msituni kufanya kazi ya siasa,”
alisema Zitto ambaye alipoulizwa na waandishi wa habari anaenda wapi, alisema
kuwa siku sio nyingi kuanzia sasa atatangaza mustakabali wake wa
kisiasa.
Hata hivyo
wachambuzi wa mambo ya siasa wanaamini kuwa mbunge huyo atajiunda na Chama cha
ACT ambacho maswahiba wake wengi ambao walitimuliwa Chadema, walienda
kukianzisha.
Wanasiasa hao
pamoja na Profesa Kitilya Mkumbo, Samson Mwigamba na wengineo wengi. Chama hicho
licha ya uchanga wake wa kisiasa, lakini kinaelezwa kuwa kina wafuasi wengi
mkoani Kigoma hasa katika Jimbo la Kigoma Mjini ambako wachambuzi wa mambo
wanasema mwanasiasa huyo ana mpango wa kwenda kugombea katika jimbo hilo ambalo
kwa sasa linashikiliwa na Peter Serukamba (CCM)
Post a Comment