Featured
    KWA HABARI NA MATANGAZO EMAIL : pbuyegu2@gmail.com ... Get a superior results by advertising with us by E- Mail us pbuyegu2@gmail.com We will bring Your Business to Light

    Featured Posts

Loading...

MWENYEKITI WA CCM IRINGA NAYE AFUNGUA PAZIA KWA KUTANGAZA NIA YA KUGOMBEA UBUNGE


PAZIA la kinyang’anyiro cha ubunge jimbo la Iringa Mjini katika Uchaguzi Mkuu wa 2015 kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM) linaelekea kufunguliwa baada ya Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Iringa, Jesca Msambatavangu kuthibitisha kuwania nafasi hiyo.
Akizungumza na wanahabari wakati akitoa taarifa ya ziara ya Katibu Mkuu wa CCM Taifa, Abdulaman Kinana mkoani hapa, Msambatavangu ambaye pia ni diwani wa Kata ya Miyomboni mjini Iringa alisema; “nitagombea.”
Alitoa jibu hilo baada ya kuulizwa na wanahabari hao kama ana azma hiyo kufuatiwa kuwepo kwa tetesi zinazomuhusisha na kinyang’anyiro hicho kinachotarajiwa kuwa na mchuano mkali ndani ya chama hicho.
Kama atatimiza azma yake hiyo, Msambatavangu atakuwa anaingia kwa mara ya pili katika kinyang’anyiro hicho ikikumbwa kwamba katika kura za maoni za chama hicho za mwaka 2010 zilizoshirikisha wagombea 12 alishika nafasi ya nne baada ya kujipatia kura 916, nyuma ya Frederick Mwakalebela aliyepata kura 3,897, Monica Mbega 2,989 na Dk Yahaya Msigwa aliyepata kura 1,217.
Wengine walioshiriki kinyanganyiro cha 2010 na kura zao kwenye mabano ni Fadhili Ngajilo (536), Addo Mwasongwe (383), Zuberi Mwachula (324), Benigus Mpete (242), Thomas Kimata (201), Chelestino Mofuga (192),  Dk Raphael Kalinga (169) na John Kiteve (136).
Katika kinyang’anyiro cha mwakani mbali na Msambatavangu aliyethibitisha kuwania nafasi hiyo wengine wanaotajwatajwa ni pamoja na Mjumbe wa Halmashauri Kuu ya CCM, Mahamudu Madenge ambaye hata hivyo amenukuliwa mara kadhaa akisema; “muda haujafika, hayo ni mambo ya mwakani kama tutakuwa hao, kazi tunayoendelea nayo sasa ni ya kuimarisha chama.”
Mbali na Madenge, makada wengine wanaotajwatajwa ndani ya chama hicho ni pamoja na Nuru Hepautwa anayefanya kazi zake zikiwemo biashara jijini Dar es Salaam na aliyekuwa Katibu Mkuu wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) Frederick Mwakalebela.
Pamoja nao yupo pia Dk Yahaya Msigwa, Fadhili Ngajilo na Mbunge wa Viti Maalumu Mkoa wa Iringa, Ritta Kabati ambaye amenukuliwa mara kadhaa akisema atajitosa katika jimbo la Iringa Mjini au Kilolo kama viti maalumu vitafutwa.
Katika mkutano wa hadhara alioufanya Januari 27, mwaka jana, Makamu Mwenyekiti wa CCM Tanzania Bara, Phillip Mangula atoa ruksa kwa wana CCM wanaotaka ubunge na udiwani katika majimbo na kata zinazoshikiliwa na wapinzani kuanza kupitapita ili kutafuta ushawishi.    
   
Wakati akitoa ruksa hiyo, Mangula aliuliza “…Iringa tulishindwaje jimbo hili, alitokea pepo gani, naomba mkemee pepo hao waliosababisha tushindwe ili 2015 turudishe  jimbo letu.”

Akizungumzia ukomo wa ruksa hiyo, Mangula alisema haihusu nafasi ya Rais na majimbo na kata zinazoongozwa na wana CCM.
“Nimeambiwa wapo walioanza kujenga makundi ndani ya chama kwa ajili ya Uchaguzi Mkuu ujao. Napenda kurudia tena ni marufuku kwa wanaCCM kuwabugudhi wanaCCM wenzao waliopo madarakani,” alisema.
Katika mkutano huo uliofanyika katika uwanja wa Mwembetogwa, Mangula alisema wanaCCM wanaojipitisha kwenye maeneo yanayoongozwa na viongozi wa CCM, wataenguliwa hata kama watashinda kura za maoni kwa ajili ya Uchaguzi Mkuu wa 2015.
Alisema kujipitisha katika maeneo wanayoyaongoza kunakibomoa chama hicho kwasababu ni chanzo kikubwa cha makundi.
“Mgogoro mkubwa ndani ya CCM ni makundi, makundi haya hujengwa kipindi cha kuelekea uchaguzi, hayana la maana zaidi ya kutubomoa. Hivi sasa nimeambiwa wapo walioanza kujenga makundi,” alisema.
Kinana na ujumbe wake wanatarajia kufanya ziara ya siku tatu mkoani Iringa ambayo pamoja na mambo mengi inalenga kukiimarisha chama hicho kwa kupokea na kuwaapisha wanachama wapya wakiwemo wanaotaka kujitoa kutoka vyama vya upinzani.
Ziara hiyo kwa mujibu wa Msambatavangu itaanzia wilayani Mufindi  Oktoba 6, mwaka huu na kuendelea katika wilaya ya Kilolo na Iringa Vijijini kabla ya kuhitimishwa Iringa Mjini
Download Our App

Post a Comment

CodeNirvana

BLOG RAFIKI

© Copyright EMMANUEL SHILATU - BREAKING NEWS BLOG
Back To Top